Tuesday, 10 February 2015

Azam yaipa Yanga saa 72



Mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL), Azam FC wameipa siku tatu Yanga kukaa kileleni mwa msimamo wa ligi hiyo msimu kabla hawajarejea katika 'nafasi yao' hiyo.
 
Mabao mawili ya winga mtokea benchini Mrisho Ngasa yaliirejesha Yanga kileleni mwa msimamo wa VPL juzi baada ya kuilaza Mtibwa Sugar 2-0 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
 
Hata hivyo, Jemedari Said, meneja wa timu ya Azam, alisema jana kuwa Yanga wana muda wa siku tatu (saa 72) tu za kukaa kileleni mwa msimamo wa ligi hiyo kwani anaamini kikosi chake kitafanya kweli katika mechi yao ya mkononi kesho dhidi ya Mtibwa na kurejea kwenye nafasi hiyo.
 
"Tuliteleza Morogoro Jumamosi na kujikuta tukilazimishwa sare dhidi ya Polisi Moro. Jumatano (kesho) tutakuwa na mechi ya kiporo dhidi ya Mtibwa Sugar. Ingawa tunakutana na timu yenye ushindani wa kweli msimu huu, ninaamini tutashinda na kurejea katika nafasi yetu," alisema Jemedari.
 
Azam FC iliiondoa Yanga kileleni baada ya kuambulia sare ya 2-2 dhidi ya Polisi Moro mjini Morogoro Jumamosi ikifikisha pointi 22, lakini ushindi wa juzi dhidi ya Mtibwa Sugar uliifanya Yanga kufikisha pointi 25 na kurejea kushika usukani.
 
Mtibwa inayonolewa na nahodha wake wa zamani, Mecky Mexime, imekuwa haipati matokeo mazuri inapocheza dhidi ya Azam FC kwenye Uwanja wa Azam, Dar es Salaam.
 
Hata hivyo, Mexime amewataka wachezaji wake kutokata tamaa kutokana na kipigo cha juzi dhidi ya mabingwa mara 24 wa Tanzania Bara, bali wageuzie akili zao katika mechi ya kesho dhidi ya Azam.
 
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

Post a Comment